Jul 25, 2012

RAIS JOHN ATTA MILLS WA GHANA AMEFARIKI DUNIA

Rais John Atta Mills

Rais John Atta Mills wa Ghana amefariki dunia ghafla jana kutokana na kuugua. Kufuatia kifo hicho, makamu wa Rais ameapishwa mara moja kushika wadhifa huo. Serikali imetangaza wiki moja ya maombolezo kitaifa.

Mills aliyekuwa na umri wa miaka 68 amefariki ikiwa ni miezi michache kabla ya kushiriki tena kwenye uchaguzi wa Urais utakaofanyika mwezi Desemba mwaka huu. Mills alikutwa na mauti akiwa hospitalini kwenye mji mkuu wa nchini hiyo Accra alipokuwa anapatiwa matibabu.

John Dramani Mahama, (katikati) rais mpya 
wa Ghana akiwa na viongozi wenziwe

Katika siku za hivi karibuni alikwenda Marekani kwa ajili ya kupima afya yake. Sababu za kifo chake bado hazijajulikana. Kwa mujibu wa katiba ya nchi hiyo, Makamu wa Rais John Dramani Mahama ndiye amechukua nafasi na tayari ameshaapishwa. Ghana, taifa la Afrika ya Magharibi inasifiwa kuwa kitovu cha demokrasia.
Mahama alikula kiapo mbele ya bunge la dharura lililoitishwa mara baada ya kifo hicho na ameahidi kulinda amani na utulivu wakati wote atakaokuwa madarakani kumalizia muhula wa mtu aliyemrithi.Tayari kiongozi huyo mpya ameshatangaza wiki nzima ya maombolezo ya kitaifa ambapo bendera zitapepea nusu mlingoti. Ana umri wa miaka 53 na alikuwa waziri wa mawasiliano kabla ya kushika wadhifa wa makamu wa Rais. Katiba hotuba yake mara baada ya kiapo Mahama alisema amepoteza mtu muhimu sana.

Mataifa yatuma rambirambi
Viongozi mbalimbali wametoa salamu za rambirambi akiwemo Rais Barack Obama wa Marekani. Obama aliichagua Ghana kuwa nchi ya kwanza kuitembelea kusini mwa jangwa la Sahara baada ya kuchukua majukumu ya urais mwaka 2009. Katika taarifa yake rasmi, amemuelezea Marehemu Mills kuwa ni mtu aliyepigana bila kuchoka kuinua maisha ya Waghana. Viongozi wengine wa mataifa ya Nigeria, Cote d'Ivoire na Togo pia wametoa rambirambi zao. Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Ban Ki Moon, naye ameusifu uongozi wake.

Rais Barack Obama wa Marekani na 
Marehemu John Atta Mills Ghana

Uvumi kuhusu maradhi yake
Vituo vya televisheni nchini Ghana GTV na TV3 vilisitisha matangazo yake ya kawaida kutangaza habari za kifo cha kiongozi huyo hapo jana. Maafisa wa serikali hawajatoa sababu za kifo chake ambacho kimemkuta siku tatu baada ya kusheherekea siku yake ya kuzaliwa.
Taarifa ya kuzorota kwa afya yake zilienea kufuatiwa safari za mara kwa mara alizofanya kwenda Marekani. Hata vyombo vya habari vya upinzani viliripoti kuwa hana uwezo wa kushiriki uchaguzi wa duru ya pili hapo mwezi Desemba. Taarifa ambazo hazina uthibitisho kutoka vyombo vya habari vya ndani ya nchi hiyo zinasema kuwa maradhi ya saratani ya koo ndiyo yaliyomuuwa.
Marehemu Mills aliwahi pia kuwa makamu wa Rais chini ya utawala wa Jerry Rawlings kiongozi wa mapinduzi ambaye baadae alichaguliwa kushika madaraka kwa kura nyingi. Aliushangaza ulimwengu kwa kuachia ngazi baada ya uchaguzi wa mwaka 2000.

No comments:

Post a Comment

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...